HEE! MAKACHO TENA, ARSENAL FC USO KWA USO NA LEICESTER CITY FC.



 Kilwa,

     Kitendawili kilichokosa jawabu Kwa muda mrefu hatimaye kimepata jawabu kwa kujulikana  nani kusonga mbele na nani kuachia ngazi katika mashindano ya Mshikamano Cup yanayoendelea kutimua vumbi katika mji Kingunge wa Kilwa kivinje.

Kitendawili hiko kimeteguliwa baada ya kujulikana timu ambazo zinaungana na Black Mob Fc pamoja na Kivinje soccer Academy katika hatua ya nusu fainali zinazotarajiwa kupigwa tarehe 24 na 25 mwezi huu.

Washika bunduki kutoka Kilwa Pande(Arsenal) walijihakikishia nafasi ya kutinga hatua ya nusu fainali kwa kuibamiza  Funguni Boys kutoka Songosongo kwa mabao 2 kwa 1 katika mechi iliyochezwa siku ya jumapili katika Dimba la ukote na kufanikiwa kutinga hatua ya nusu fainali huku mabingwa watetezi Leicester City Fc wakiilaza na viatu Al- qaeda Fc kutoka Njianne kwa kipigo cha goli 3 kwa 1 katika  mtanange uliopigwa mapema hii leo.


Mchezaji mwandamizi wa Leicester City Fc Mustafa Makacho ameendelea kuonyesha makali yake ya kucheka na nyavu za timu pinzani baada ya kuisaidia timu yake kwa kuifungia goli 1 katika ushindi wa magoli 3 na kumfanya kufikisha magoli 6 katika mashindano hayo.

Mustafa Makacho akiwa ameshika mpira wake aliokabidhiwa baada ya kufunga goli 3 katika moja ya mechi alizocheza katika Mshikamano Cup.


Kwa matokeo hayo Arsenal Fc, Leicester City Fc wanaungana na Black Mob Fc (Makuzi) na Kivinje Soccer Academy katika hatua ya Nusu fainali inayoenda kuanza mapema siku ya Alhamisi.

. RATIBA KAMILI HATUA YA NUSU FAINALI MSHIKAMANO CUP.
_________________________________________
Tarehe: 24/08/2017
Mechi:  Black Mob Fc (Makuzi) V/s Kivinje Soccer Academy
Muda : Kuanzia majira ya saa 10 jioni
Uwanja: Ukote Stadium
Mahali: Kilwa Kivinje
_________________________________________
Tarehe: 25/08/2017
Mechi:  Arsenal Fc V/s Leicester City Fc
Muda : Kuanzia majira ya saa 10 jioni
Uwanja: Ukote Stadium
Mahali: Kilwa Kivinje

Mshikamano Cup ni ligi ya mpira wa miguu iliyoanzishwa rasmi mwaka 2012 na hufanyika kila mwaka mwezi wa 7 katika mji mkongwe wa Kilwa Kivinje katika uwanja wa Ukote, Ni mashindano ambayo yamejizolea umaarufu mkubwa katika wilaya ya kilwa na viunga vyake kwa kuibua vipaji, kujenga mshikamano miongoni mwa wapenzi wa kandanda  sanjali na kutoa ajira kwa vijana.



 
Previous
Next Post »