NAIBU WAZIRI KAKUNDA AFANYA ZIARA KILWA, ATOA ONYO KALI.



Kilwa,

Naibu waziri ofisi ya Rais TAMISEMI Mhe. George joseph Kakunda amesema serikali itawachukulia hatua kali za kisheria walimu wakuu na wote ambao watabainika kutengeneza uhamisho bandia kwa wanafunzi wa kike kwa dhumuni la kwenda kuwaozesha.

 Ameyasema hayo alipokua akizungumza na baadhi ya watumishi wa halmashauri ya wilaya ya Kilwa waliojitokeza katika ukumbi wa jumba la maendeleo mjini Kilwa masoko.

Naibu waziri amesema wale wote ambao watabainika kushiriki katika udanganyifu au njia nyingine yeyote ambayo itatumika kukatiza masomo kwa wasichana basi adhabu kali itachukuliwa juu yao ikiwemo kifungo cha miaka thelathini jela.

Amesema kuna baadhi ya wazazi wamekua wakishirikiana na walimu wakuu kutengeneza  uhamisho ambao unaonyesha kua mwanafunzi anahamia shule Fulani lakini mwisho wa siku anaenda kuozeshwa bila kufika kule ambako uhamisho unaonyesha.

“Nasema wale wote ambao watakutwa na hatia ya kukatisha masomo kwa wasichana kwa ajili ya kuwaozesha basi kifungo cha miaka thelethini kitamuhusu kuanzia mzazi, mshenga, shekhe au padri atakaefungisha ndoa hio na wale wote watakao enda katika sherehe hio watafungwa miaka thelathini jela.” Alisema naibu waziri 

Pia naibu waziri amezitaka mahakama kuharakisha hukumu kwa wale wote ambao watakutwa na hatia ya kukatisha masomo kwa kuwatia mimba wanafunzi.

Aidha naibu waziri ameipongeza Halmashauri ya wilaya ya Kilwa chini ya Mkurugenzi wake Bw. Zablon Bugingo Kwa kuibua na kusimamia miradi mbalimbali ya maendeleo ambayo imekua na manufaa na tija kwa wananchi.

Akihitimisha mazungumzo hayo mkuu wa wilaya ya Kilwa Mh. Christopher Ngubiagai ameahidi kuyafanyia kazi maagizo na ushauri alioutoa naibu waziri kwa kushirikiana na wataalamu mbalimbali kutoka  halmashauri ya wilaya ya Kilwa.

 Akiwa wilayani Kilwa niabu waziri alitembelea miradi mbalimbali ya kimaendeleo ikiwemo mradi wa uoteshaji wa miche ya mikorosho ya kisasa, mradi ambao unasimamiwa na halmashauri ya wilaya ya Kilwa.
Mkurugenzi wa halmashauri ya Kilwa Zablon Bugingo kulia akitoamaelezo ya mradi mkubwa wa uoteshaji wa miche ya korosho kwa Naibu waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI George Kakunda alipofanya ziara leo Wilayani humo kushoto ni Mkuu wa wilaya hiyo Christopher Ngubiagai . 
Halmashauri  ya wilaya ya Kilwa kwa kushirikiana na watalamu mbalimbali inaotesha jumla ya miche milioni moja ya mikorosho ya kisasa ambayo inatarajiwa kugawiwa bure kwa wakulima ikiwa ni njia ya kuongeza uzalishaji wa zao hilo  sambamba na kuongeza  pato la halmashauri. 
 
Kwa sasa wilaya ya Kilwa ina jumla ya mikorosho laki sita tu ambayo msimu wa 2016/2017 iliingiza kiasi cha shilingi Bilioni kumi na tatu za kitanzania na halmashauri ilipata zaidi ya shilingi milioni 220 baada ya mgawanyo.
Picha ikionyesha viriba vya kuoteshea miche ya korosho



Previous
Next Post »