Kilwa,
Timu ya Kilwa youth soccer academy imeibuka
na ushindi mwembamba wa goli moja kwa sifuri dhidi ya Tamofa fc kutoka mji mkongwe wa kihistoria Kilwa kisiwani ikiwa ni muendelezo wa ligi
daraja la nne ngazi ya wilaya kituo cha masoko.
Mtanange huo uliotawaliwa na kasi ya hali ya juu umepigwa mapema leo katika uwanja wa mwenge (Taifa) mjini
Kilwa Masoko huku ukishuhudiwa na idadi kubwa ya wapenzi na wadau wa soka wilayani hapo.
Timu zote zilionyesha umahiri wa hali ya juu kwa
kucheza mchezo wa kujiamini na kushambuliana kwa zamu hali ambayo
ilipelekea timu hizo ziende mapumziko zikiwa hazijaruhusu nyavu kutikiswa.
Zikiwa zimesalia
takribani dakika kumi ta tano kumalizika kwa pambano hilo, Mwalimu wa Kilwa
Youth soccer academy alifanya mabadiliko
ya kiufundi kwa kumtoa mchezaji Nurdin
Bakari na kumuingiza Mohamed Hafidhi
ambaye alifunga goli pekee katika mtanange huo katika dakika za lala
salama .
Katika mechi ya
ufunguzi wa ligi hio iliyopigwa siku ya
juma tano katika uwanja wa mwenge (Taifa) mjini Kilwa timu ya Ngome fc kutoka
Kilwa masoko ilichoshana nguvu na Tamofa Fc kutoka Kilwa kisiwani kwa sare ya
magoli mawili kwa mawili huku Mihina Fc wao wakitoka suluhu dhidi ya Al qaeda
katika mtanage wa pili uliorindima siku ya Alhamisi.
Ligi hiyo inatarajiwa
kuendelea tena kesho kwa mchezo mmoja ambapo majira ya saa kumi jioni timu ya
Kichanga chui Fc itakua uwanjani wakimenyana na Al qaeda Fc zote kutoka Mjini
Kilwa Masoko.
Ligi daraja la nne
ngazi ya wilaya, wilaya ya Kilwa inajumuisha jumla ya timu kumi na nne ambazo
zimegawanywa katika vituo vitatu ambavyo ni Masoko, Njia nne na Somanga ambapo
kituo cha masoko kina timu sita, njia nne timu nne na somanga timu nne.
Baada ya kukamilika kwa
michezo yote ya makundi mshindi wa kwanza kutoka katika vituo vya njia nne na somanga
watamenyana na washindi wa kwanza na wa pili kutoka kituo cha masoko ambapo
timu mbili zitakazo shinda zitakua
zimefuzu kwenda ngazi ya mkoa.
Sign up here with your email
ConversionConversion EmoticonEmoticon