KINYONGA KUCHELE, MAMBO KIDIGITALI ZAIDI.




Kilwa, 
Hospitali ya wilaya ya kilwa (kinyonga) imefanya mabadiliko kwa kutoka katika mfumo wa analogia na kuhamia digitali katika utaratibu wa kusaini katika daftari la mahudhurio kwa watumishi pamoja na mfumo wa kuhifadhi taarifa hospitali hapo. 

Mabadiliko hayo yamekuja siku chache baada ya kufungiwa mifumo maalumu ya kielektroniki ya kuchukua taarifa za mahudhurio kwa watumishi kwa kutumia kifaa kijulikanacho kwa jina la Biometrics Attendance Reader pamoja na mfumo wa taifa wa kuhifadhi taarifa Hospitalini GoTHoMIS.

Biometrics attendence reader ni kifaa cha kielekroniki chenye uwezo wa kurekodi na kutunza kumbukumbu za mtumishi kuanzia jina, tarehe, saa, na dakika ambayo amesaini wakati wa kuingia na kutoka kazini na mengineyo mengi  baada ya kuweka alama ya kidole (finger print) katika kifaa hiko.

 GoTHoMIS ni mfumo ambao unahifadhi taarifa za mgonjwa kielektroniki toka anaporipoti mapokezi mpaka mwisho anaepoenda kuchukua dawa, bila kuhusisha matumizi ya daftrari kama awali. 

Kupitia mfumo wa GoTHoMIS taarifa za mgonjwa toka mapokezi zinatumwa moja kwa moja mpaka kwa Keshia ambapo atalipia na kupatiwa risiti ambayo itamruhusu kwenda kuonana na Daktari, ambapo atakuta baadhi ya taarifa zake za awali zimefika.

Baada ya kuonana na Daktari maagizo yatakayotolewa na Daktari yatakua yame kwisha fika sehemu husika ambayo mgonjwa ataelekezwa aende, kwa mfano kama atahitajika akapate vipimo maabara, pumzishwe wodini, au apelekwe kwenye chumba cha upasuaji nk taarifa zitakua zimesha fika sehemu husika.

Baada ya kumaliza matibabu kumbukumbu za mgonjwa zitabaki katika mfumo huo uliofungwa hospitali hapo na iwapo atarudi kwa siku nyingine atataja jina lake tu,na  taarifa zake za awali zitaonekana  kabla ya kuendelea na  matibabu.

Kupitia mifumo hio mipya uongozi utapata kuona na kujua orodha ya watumishi ambao ni watoro kazini, wanaochelewa kufika na wanao wahi kutoka kabla ya muda uliopangwa pamoja na kuwa na kumbukumbu sahihi za taarifa za wagonjwa, matumizi ya dawa pamoja mapato ya kila siku hospitalini hapo.
Picha ya Biometrics Attendance Reader, kifaa kinacho tumika kuchukua taarifa za mahudhurio kwa watumishi kwa kutumia alama ya kidole.


Akionyesha kufurahishwa na mifumo hio mipya Katibu wa afya Hospitali ya wilaya Kinyonga Bi. Zabibu Uledi amesema mifumo hio mipya itasaidia sana kurahisisha upatikanaji wa takwimu za mahudhurio ya watumishi, wagonjwa na kumbukumbu zingine kwa haraka sana ukifananisha na mifumo iliokua ukitumika awali.

Aidha Bi. Zabibu amewaomba watumishi watumie mifumo hio kwa umakini na uangalifu ili iweze kudumu kwa muda mrefu na hatimae kuleta matokeo chanya.
“Ni waombe tu watumishi wawe waangalifu kwenye utumiaji wa mifumo hii ili iweze kudumu kwa muda mrefu.” alisisitiza.

Nae Bi.Veronica akizungumza kwa niaba ya watumishi wengine wa hospitali ya kinyonga amesema  wanashukuru kwa mifumo hio mipya kwani ni mizuri na itasaidia kuondoa msongamano muda wa kusaini kwa kua mfumo huo unafanya kazi kielektroniki zaidi pia mfumo wa GoTHoMIS  utasaidia upatikanaji wa kumbukumbu sahihi za wagonjwa hospitalini hapo.

Mfumo wa kielektroniki wa GoTHoMIS umekwisha anza kutumika hospitali hapo majuma kadhaa yaliyopita licha ya kukumbwa na changamoto kubwa ya baadhi ya watumishi hospitali hapo kutokua na ujuzi wa kutumia kompyuta wakati mfumo kusaini kwa kutumia alama za vidole (finger print) unatarajiwa kuanza kutumika siku chache zijazo. 

Hospitali ya kinyonga ni taasisi ya pili kunufaika na mfumo huo wa kidigitali wa kuchukua taarifa za mahudhurio kwa watumishi baada ya idara mbalimbali zilizopo katika makao makuu ya halmashauri ya wilaya ya kilwa kunufaika na mfumo huo.

Halmashauri ya wilaya ya kilwa ni miongoni mwa wilaya chache Tanzania ambazo zinatumia mfumo wa kidigitali wa kuchukua rekodi za mahudhurio kwa watumishi wake pamoja mfumo wa taifa wa kuhifadhi taarifa Hospitalini (GoTHoMIS).
Previous
Next Post »